MAMLAKA YA WAZIRI NA UHURU WA KUJIELEZA



NA MARYAM NASSOR,

HARAKATI  za kupigania sheria  nzuri za Habari Zanzibar  zimeanza kwa muda  mrefu  takribani miongo miwili  sasa.

Harakati hizo, zimekuwa zikifanywa na waandishi  wa Habari na wadau mbali mbali wa Habari  nchini, kupigania kupata  sheria nzuri ya habari inakayotoa uhuru wa kujieleza na haki ya kupata taarifa.

Uhuru wa Habari , umeelezwa ndani ya  Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha  18  ambacho  kinasomeka: (1)  bila ya kuathiri sheria nyengine za nchi, kila mtu anayo haki na uhuru wa kutoa maoni (kujieleza)  -  kutafuta, kupokea na kusambaza Habari   na mawazo yake  kupitia  chombo  chochote cha Habari bila ya kujali mipaka  ya nchi  na pia anayo haki  na uhuru wa kutoingiliwa  mawasiliano yake.

 Katika  kifungu hicho , sentensi inayosema “bila ya kuathiri sheria nyingine za nchi  inanyima uhuru wa kujieleza , kutafuta  na kusambaza Habari  kwa sababu kinaruhusu kutungwa kwa sheria nyingine ambazo kwa namna moja ama nyingine zinaweza kuminya uhuru wa habari.

 Na kwa bahati mbaya , Baraza la Wawakilishi  limetunga sheria mbaya  ambazo zinakwaza uhuru wa Habari na uhuru wa kujieleza kama Kifungu cha 30 kinachompa mamlaka makubwa  Waziri wa Habari kufungia  chombo cha Habari. 

Kifungu hicho kinasema “  endapo  Waziri  ataona kuwa ni kwa manufaa ya umma  na kwa maslahi ya amani na utulivu, anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti hilo  na litakoma kuchapishwa kuanzia tarehe hiyo”.

Januari 2021 Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ilikifungia kituo cha Utangazaji cha Wasafi TV kwa muda wa miezi sita  kuanzia January  06  mpaka Juni 2021 kwa kukiuka taratibu za utangazaji.

Hiyo, ilikuwa ni mara ya pili kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, kufungia kituo hicho , mwezi Septemba 2023 Wasafi FM ilifungiwa kwa siku saba kuanzia  Septemba 12 hadi Septemba 18 makosa yakiwa ni ukiukwaji wa kanuni za mawasiliano ya kieletroniki na Posta katika utangazaji wa radio.

Kwa wadau wa  vyombo vya Habari, matukio ya namna hii ndio yanaakisi uwepo wa sheria  zinazotoa  mamlaka makubwa kwa taasisi zinazosimamia vyombo vya  Habari, wakati mwingine zikitoa adhabu kubwa ukilinganisha na lile linalo tafsiriwa kuwa ni kosa. 

Mwanasheria Ali Amour kutoka Ofisi ya  Mwendesha Mashtaka wa Serikali Zanzibar,  anasema  ni kweli kuwepo kwa kifungu  ambacho kinampa  mamlaka makubwa Waziri wa Habari , kinanyima uhuru wa vyombo vya Habari na kujieleza kutokana na kuwa hiyo sheria imepitwa na wakati.

Amesema kuwa, mamlaka makubwa aliyopewa Waziri  kapewa kisheria akiyatumia vibaya , basi  yanaweza kuathiri uhuru wa Habari na kujieleza. 

Aidha amesema kuwa, sheria ilipaswa iorodheshe mazingira gani yakitokezea ndio,  anaweza akafanya maamuzi hayo, isiwe tu sheria inampa maamuzi hayo, moja kwa moja anaweza kufungia chombo cha Habari kwa dhana tu ya kulinda  maslahi ya Umma..

“Lakini pia  Waziri wa Habari anayeteuliwa  ana taaluma gani ya Habari ili kujua ni kweli chombo cha Habari kimeenda kinyume na maadili ya habari, hivyo ni vizuri Waziri wa Habari  awe mwanahabari” ameshauri mwanasheria huyo.

Nae Mwandishi wa Habari wa Zanzibar Cable Television Malik Shaharan, amesema kuwepo kwa sheria kandamizi kama hizo, zinanyima uhuru wa Habari na kujieleza kwani  vyombo vingi vya habari vimekuwa vikipata misuko suko kutokana na sheria mbaya ambazo zimepitwa na wakati.

 Amesema kuwa, ni vyema sheria mbaya kama hizo zikabadilishwa ili kuvipa uhuru vyombo vya Habari  na jamii kutoa maoni yao na uhuru wa kupata taarifa.

 Chombo cha Habari kinatakiwa kufungiwa baada ya mahakama kijiridhisha na sio kwa Waziri kufanya maamuzi  makubwa kama hayo na kusababisha  kuviza uhuru wa  Habari” anasema Malick.

 Shadida Mohamed kutoka Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania - THRDC anasema kuwa madhara ya kifungu hicho ni makubwa, kinaweza kutumika kama chombo cha  kudhibiti  uhuru wa Habari hasa kwa magazeti yanayokosoa Serikali  au viongozi wake.

Anasema kuwa, hatari ya kifungu hicho cha 30 cha sheria ya wakala wa habari, magazeti na vijarida na. 5 ya mwaka 1988 ni kule kumpa  Waziri  mamlaka ya kufungia gazeti kwa maslahi ya taifa anapoona inafaa. Waziri anaweza kuyatumia vibaya mamlaka hayo kwa maslahi binafsi au ya kisiasa.

“Kukuza uhuru wa Habari , sheria isisitize kuheshimu haki za msingi za uhuru wa kujieleza na kupata taarifa kutoka kwa vyombo vya habari  bila ya kuingiliwa na Waziri “ ameshauri .

 Mkurugenzi wa Chama cha Wandishi wa Habari  Wanawake Tanzania Zanzibar -TAMWA ZNZ  Dk Mzuri Issa amesema chombo cha habari kinatakiwa kufungiwa kama ikibidi na mahakama kudhibitisha  sheria zimekiukwa na sio, kwa mamlaka  makubwa ya Waziri wa Habari.

Amesema kuwa,  sheria hiyo imempa mamlaka makubwa Waziri inatakiwa ibadilishwe kwa ustawi wa vyombo vya Habari” Kumpa mamlaka makubwa Waziri kama hayo  ni kunyima uhuru wa vyombo vya Habari nchini, ndio maana Waandishi wa Habari wa Zanzibar hawaandiki Habari za uchunguzi kwa hofu ya kufungiwa ,” anasema Dk Mzuri.   

*******

 

No comments

Powered by Blogger.