Wadau washauri Michezo itumike kama njia ya kujikinga na Ukatili wa Kijinsia.

 


 NA MARYAM NASSOR,

Sera ya Michezo ya  Zanzibar ya mwaka 2018, imetamka wazi nia njema ya  Serikali , katika kuhakikisha Usawa wa kijinsia katika Michezo.

Haya hivyo, Sera hiyo haifanyi kazi ipasavyo, kama  wachezaji  wakike na kiume hawatopewa Elimu ya kujikinga na vitendo vya Udhalilishaji katika  Michezo.

Kwa mujibu wa ripoti  mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto, UNICEF  ya mwaka 2024,Inaonesha kuwa   Zaidi ya wasichana na wavulana milioni 370 ni waathirika wa ukatili wa kijinsia duniani kote, kabla ya kutimia  umri wa miaka 18.

Kulingana na ripoti hiyo,  inaonesha kwamba msichana mmoja kati ya wanne ameathirika na aina hii ya unyanyasaji mbali na ule wa kimtandao au wa maneno , idadi ya wasichana na wanawake  waliyoathirika duniani kote imeongezeka hadi  kufikia  milioni 650 , huku ikisisitiza umuhimu wa  kuchukua mikakati ya dharura kukabiliana na  hali hiyo.

 Hivyo,Ipo haya ya kuitumia michezo kama njia ya kujikinga na vitendo vya ukatili na Udhalilishaji, kwa wasichana na wavulana  Kwani vitendo hivyo, Kila kukicha vinaonekana kuongezeka.

Akizungumza na mwandishi wa makala hii, mchezaji  wa mpira wa miguu  timu ya Wanawake ya Worrious,  Saada  Saidi, amesema kwenye michezo kunatokea vitendo vingi vya Ukatili na Udhalilishaji wa Kijinsia hasa kwa wasichana lakini pia na wavulana .

Amesema kuwa, Ipo haja Kwa wachezaji kupewa elimu ya Udhalilishaji na ukatili wa kijinsia kwani madhara ya vitendo hivyo,  huwa na athari kubwa na  za kudumu kwa waathirika wa vitendo hivyo.

Aidha amesema kuwa, ukatili wa kijinsia dhidi ya Watoto ni  janga,  na linaleta majeraha makubwa na  ya kudumu,ambapo waathirika hulibeba hadi utuuzima.

"Sisi wachezaji wa mpira wa miguu, tunanza kucheza mpira tukiwa wadogo, na hatupewi elimu ya kujikinga na Udhalilishaji Kwa hivyo, hata ukifanyiwa Udhalilishaji na kocha wako hujui kama umedhalilishwa" amesema Saada.

Aidha amesema kuwa, ni muhimu wachezaji wakapewa elimu ya kujikinga na vitendo vya Udhalilishaji kupitia michezo kwani, vitendo hivyo  vimekuwa vikiwarudisha nyuma wachezaji  kufikia ndoto zao.

“ Wachezaji wengi wamekuwa wakiacha kucheza na kufikia ndoto zao,  kwenye michezo kutokana na udhalilishaji michezoni” amesema mchezaji huyo anaesakata kabumbu katika timu ya wanawake ya  Warrious Zanzibar.

Abubakar Said, ni mchezaji wa  mpira wa miguu Timu ya Muembe Ladu FC, amesema  michezo  ni afya, ni pesa  lakini pia ndio sekta inayoongoza kutoa ajira Duniani kwa vijana, hivyo ni lazima wachezaji wa soka wakapewa elimu ya kujikinga na vitendo viovu kama udhalilishaji na ukatili wa kijinsia.

Amesema kuwa,  ni vyema  watoto wakaitumia  michezo kama njia ya kujikinga na vitendo vya Udhalilishaji, kwani vinonekana kuongezeka siku hadi siku.

Nae, mchezaji wa mpira  wa miguu kutoka Timu ya New Generation, Faidha Juma amesema  ipo haja ya kuitumia michezo kama njia ya kuwalinda watoto, dhidi ya vitendo vya Udhalilishaji.

Aidha, ametoa wito Kwa Jamii na wazazi Kwa ujumla, kuwaruhusu watoto wao kushiriki michezo,  mbali mbali tokea wako wadogo ili kuwasaidia  kukuza akili za Watoto, na kuwafanya wawe wepesi  katika kujifunza.

"Wazazi tuwaruhusu watoto kushiriki michezo mbali mbali , ili kuwajengea uwezo wa  kimwili na kiakili ili  wapate kujilinda na vitendo vya Udhalilishaji Kwani wakiipata elimu hiyo kupitia michezo itawasaidia kujilinda " ameshauri mchezaji huyo.

 

Nasra Juma Mohamed ni Naibu kamishna wa Timu ya Uhamiaji Zanzibar na kocha wa Mpira wa Miguu, amesema ipo haja Kwa sasa  kutokana na hali ilivyo, kuitumia michezo kama njia ya kujikinga na kujilinda na vitendo vya Udhalilishaji kwa watoto.

Amesema kuwa, haiwezi  kupita  siku bila ya  kusikia watoto wamebakwa au wamelawitiwa, hivyo ni lazima tutafute njia mbadala ya kujikinga na kukabiliana na hali hiyo..

"Michezo ni njia moja wapo ya kujikinga na kuwalinda watoto wetu na vitendo vya Udhalilishaji kwani Watoto wanaoshiriki michezo huwa na uwezo mkubwa wa kujihami ukilinganisha na wale  wasio shiriki michezo " amesema Kocha Nasra.

Aidha amesema kuwa, tafiti zinaonesha Kila kwenye watoto watano mmoja kakumbwa na vitendo vya Udhalilishaji wa kijinsia.

 Nae, Kamishna wa Baraza la Michezo Zanzibar, Mohamed Makame amesema ni vyema  Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, ikapanga muda maalumu mashuleni  wanafunzi wakafundishwa michezo mbali mbali wakiwa bado wadogo.

Amesema kuwa, hiyo itasaidia kuibua vipaji lakini pia , watoto hao kufundishwa michezo kama njia ya kujikinga na vitendo vya Udhalilishaji ambavyo  vimekuwa vikiongezeka  kila uchao.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Riziki Pembe Juma, alipokuwa akizindua Mpango Mkakati Jumuishi wa Jinsia katika Michezo Zanzibar wa mwaka 2024/25-2028/29.alisema kuwa Mpango huo, utumike Kama  Muongozo wa kujilinda   na vitendo vya udhalilishaji Michezoni.

Amesema kuwa, Mpango huo umezingatia Usawa wa kijinsia, na Ujumuishi  ili kusaidia Utekelezaji wa Dira ya Michezo ya Zanzibar ya mwaka  2018.

Aidha, aliishauri Jamii na wanamichezo kuusoma Mpango Mkakati huo, ili kuuelewa, na wanamichezo kuutumia katika kujilinda na  vitendo vya Udhalilishaji wakiwa  kwenye michezo.

Khairat Haji, ni Afisa Programu ya  Michezo Kwa Maendeleo kutoka Chama Cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar, (TAMWA ZNZ) akisoma ripoti ya matukio ya Ukatili na Udhalilishaji katika  maadhimisho  ya  siku 16 za kupinga Udhalilishaji ,aliwataka Watoto wakike na wasichana  kuitumia michezo kama njia moja wapo ya kujikinga na vitendo vya udhalilishaji.`

Akisoma, ripoti ya majumuisho ya vitendo vya ukatili na Udhalilishaji , kutoka January  hadi Oktoba mwaka huu, alisema   takwimu za kesi hizo zinaonesha hali ya kutisha  kwa kuongezeka kwa vitendo hivyo, kati ya  kesi 1,582  za ukatili wa kijinsia ziliripotiwa na waathirika Watoto walikuwa ni 1,337 kati ya hao wasichana walikuwa ni 1,095 na wavulana 242.

Aidha alisema kuwa, kesi 693 zilihusisha Watoto wa  umri  kati ya miaka 15 hadi16 huku , akitanabahisha kuwa vitendo  hivyo hufanyika kati ya saa 9:00 na saa tatu usiku , wakati ambao Watoto wengi  wapo mazingira ya nyumbani ambapo kuna usalama, huku wilaya  ya Magharibi ‘B’ikiongoza kwa matukio  mengi ya udhalilishaji yakiwa ni  386, ikifuatiwa na wilaya ya Mjini  Unguja ambayo iliripoti kesi   344 na Magharibi  ‘A’  ikiwa na kesi 373.

                                      

No comments

Powered by Blogger.