TAMWA-ZANZIBAR: ''WANAWAKE JITOKEZENI 2025 MSIJALI VITISHO''

 





NA MARYAM NASSOR, ZANZIBAR.

MKURUGENZI wa Chama cha wandishi wa habari wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar Dk. Mzuri Issa Ali, amewataka wanawake kujitokeza kwa wingi  kugombea nafasi mbali mbali za uongozi majimboni,  ili kuongeza ushiriki wao bila ya kuogopa vitisho.

Dk. Mzuri ameyasema hayo leo Oktoba 1, 2024 ukumbi wa mikutano wa chama hicho Tunguu Unguja, katika kikao cha kueleza namna gani  wanawake  watapata ulinzi dhidi ya ukatili wa kijinsia  mitandaoni, kupitia mradi wa wakuwawezesha waandishi wa habari vijana.

Amesema kuwa, hamu yao ni kuona wanawake wengi  wanaingia majimboni kugombea nafasi mbali mbali, lakini suala la udhalilishaji mitandaoni, linawarudisha nyuma.

“Jamii inaamii mtu akitaka kugombea nafasi ya uongozi ni lazima awe msafi kwa asilimia 100, lakini mwanamke ni binadamu na  hakosi mapungufu,’’alisema.

Amesema kuwa, moja kati ya kikwazo kikubwa kwa wanawake katika kugombea ni vitisho kutoka wagombea wanaume.

‘’Wanawake musiogope kujitokeza kugombea, kwani wamekuwa kidogo katika kugombea nafasi za uongozi, wakisumbuliwa na ukatili wa  wa kijinsia mitandaoni lakini musivunjike moyo,’’alifafanua.

Afisa kutoka Mamlaka ya kuzuia rushwa na uhuhumu wa uchumi Zanzibar ‘ZAECA’ Yussuf Juma Suleiman, amesema moja kati ya vikwanzo  vinavyowarudisha nyuma  wanawake katika kugombea nafasi za uongozi ni rushwa ya ngono.

Amesema kuwa, kabla wanawake hawajaingia katika kugombea nafasi za uongozi, ni vizuri kupewa elimu ya uraia, ili kujua miiko na misingi ya uongozi, ili wasiwe na mwanya wa kutoa rushwa.

Aidha amesema kuwa, serikali ya Mapinduzi Zanzibar imepitisha sheria mpya ya kuzuia rushwa na uhujumu wa uchumi, sheria namba 5 ya mwaka 2023, kifungu cha 53.

Amesema, kifungu hicho kimeharamisha rushwa ya ngono, kwa kukataza mtu yoyote kushawishi, kuahidi kufanya ngono na adhabu yake ni kifungo kisichopungua miaka saba na kisichozidi miaka 10.

“Rushwa ya ngono ni uhalifu kama ulivyo mwingine, na serikali imeazisha sheria ili kukabiliana nayo, lakini wandishi wa habari toeni elimu ili wanawake wanaotia nia wasiwe ni mwanya wa kutokea rushwa,’’ alisema.

Nae Afisa sheria Mwandamizi kutoka ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, Abdul-razak Said Ali amesema   serikali imekuwa ikichukua jitihada mbali mbali, katika kumuwezesha mwanamke kugombania nafasi za uongozi ili kuongeza ushiriki wao.



Alisema kuwa, moja ya hatua iliyochukuliwa na serikali ni kuongeza kifungu katika sheria ya vyama vya siasa nambari 1 ya mwaka 2024, kifungu namba 10 (c) ndani ya marekebisho, kinatoa masharti yanayohusiana na uanzishwaji wa dawati la kijinsia na ushirikishwaji wa jinsia na jamii.

Na washiriki wa mkutano huo Mwalim Mwatima Issa, Rashid alisema wandishi wa habari wanatakiwa kujipa kipaumbele katika kufanya kazi zao.

Nae mshiriki Nusra Shabani aliuliza kwanini vyama vidogo vya siasa, havipewi ruzuku ili kuviwezesha vishiriki kikamilifu katika uchaguzi.

                Mwisho 

 

No comments

Powered by Blogger.