FAWE ZANZIBAR , UN WOMEN ZINAVYOWAWEZESHA WANAWAKE KUFIKIA KIZAZI CHENYE HAKI NA USAWA KIUCHUMI.
NA MWANDISHI WETU,
FAWE Zanzibar, UN Women zinavyowawezesha Wanawake
kufikia kizazi chenye usawa kiuchumi.
KATIKA jitihada za kuhakikisha Tanzania inafanikisha
utekelezaji wa malengo manne ya kizazi
chenye usawa wa kiuchumi, jukwaa la wanawake wanaelimu wa Afrika, Zanzibar
(FAWE Zanzibar) inawezesha wanawake Zanzibar kukabiliana na vikwazo kiuchumi.
Kwa kushirikiana na UN women Tanzania, FAWE Zanzibar
inachangia ufikiaji wa malengo hayo kupitia utekelezaji wa mpaango wa pamoja wa
umoja wa mataifa wa kuharakisha maendeleo ya kiuchumi kwa wanawake Vijijini
(JPRWEE) unalengo la kuhakikisha ustawi wa Wanawake Vijijini na haki zao.
Aidha, utekelezaji wa mpango huo unaenda sambamba na
utoaji wa mafunzo kwa wanawake ili kusaidia kupata ujuzi wa biashara,
elimu ya kifedha, pamoja na fursa za
kupata mikopo ili kuanzisha na kukuza biashara zao.
Miongoni mwa mafanikio yaliyoelezwa na wanufaika wa mradi huo, ambao
unatekelezwa mkoa wa kusini Unguja ni kuongezeka kwa ajira, hali iliyoboresha
kipato cha kaya na kupunguza utegemezi kwa waume.
Walisema, mradi huo umewawezesha wanawake wengi
kuanzisha biashara ndogo ndogo, kama
vile kukuza biashara za kilimo, ushonaji na uzalishaji wa bidhaa za nyumbani
kama vile sabuni na mishumaa.
Si wanawake tu walionufaika na uwepo wa mradi huu,
hata kwa wanaume pia mradi huu umebainika kuwa ufunguo wa kuwafikia haki na
usawa wa kiuchumi.
Assa Hassan Khamis ni mwanakikundi cha upishi, SUBIRA
INA MALIPO kutoka shehia ya Uzi Mkoa wa kusini Unguja, alisema'' mafanikio
ninayojivunia ni kupata mafunzo ya
upishi ambayo yamenisaidia katika kujiajiri mimi mwenyewe na kumsaidia mke
wangu majukumu ya kupika akiwa na tatizo''
alisema.
Nae, Mwakombo Nyange Shamata kutoka kikundi cha UROA
SACCOS, alisema wamepata mikopo ambayo imewasaidia kununua vifaa vya ukulima wa
mwani ambao ndio wanaoutegemea kwa kuendesha maisha yao ya kila siku.
''Tumepata mafanikio makubwa katika mradi huu kwani
tumepata mikopo ambayo imetufanya tununue vifaa vya ukulima wa mwani ambao ndio
rasilimali ya uchumi wetu'' alieleza mwakombo huku akitabasamu.
Kwa upande wa shida Hassan Mambo, kutoka kikundi cha
TUPENDANE kilichopo Uroa wilaya ya kati
Unguja, alisema kupitia mafunzo ya usimamizi wa fedha , na kupanga matumizi
mazuri , hali iliyosaidia biashara nyingi kukua.
'' Mradi umetusaidia sana sisi wanawake kufanya
shughuli zetu za kiuchumi ikiwemo kuweka na kukopa jambo ambalo lilitusaidia
kujikwamua na changamoto ya kifedha tunapopatwa na matatizo '' alisema
mwanakikundi huo.
Licha ya juhudi kadhaa zinazochukuliwa, lakini
Zanzibar bado inakabiliwa na changamoto ya soko la mwani.
''Serikali inasema kilo ya mwani inunuliwe kwa
shilingi 1,000 lakini wanunuzi hununua kwa shilingi 700, hatupati chochote
zaidi ya maumivu'' alisema Arabia Fauzi Pandu mwanakikundi cha mwani cha
USALAMA WETU kutoka Jambiani wilaya ya Kusini Unguja.
Afisa Tathimini na ufuatiliaji FAWE Zanzibar, Shaban
Suleiman alisema mradi una wawezesha wanawake wa vijijini kiuchumi ili kuona
wanapata maendeleo ya kiuchumi katika maisha yao.
'' Tumewapatia elimu ya ujasiriamali na elimu ya
biashara ili waweze kufanya shughuli zao
za kiuchumi katika kujikusanya kwa pamoja na tumewahamasisha kuchukua mikopo Serikalini'' alisema Shaban.
Silivia Lanzarini, Afisa Ufuatiliaji na Matalam wa
program kutoka UN women akitembelea wanufaika hao aliwashauri wajasiriamali
wanawake kuweka akiba ya fedha kwenye vikundi vyao, ili waweze kupata mikopo
zaidi itakayosaidia kutatua changamoto ndani ya vikundi vyao na jamii kwa
inayowazunguka.
''Nimefurahi kukutana nanyi katika kuona
mafanikio na changamoto zenu katika mradi huu, ni matumai yangu mafanikio
muliyoyapata munayafurahia'' Silvia aliwaeleza huku akionesha
kufurahishwa na juhudi zao.
Programu ya kizazi chenye usawa( 2021-2026)
inajumuisha afua nne ikiwemo kuanzisha na kuendeleza vituo vya malezi na makuzi
ya watoto, kuongeza uwekezaji katika
usambazaji maji, umeme na nishati mbadala yenye kukuza mazingira na
matumizi ya teknolojia yenye gharama nafuu, kuongeza kazi zenye staha kwa
kuendeleza biashara na urasimishaji
wa biashara za wanawake, na kuboresha upatikanaji na matumizi ya teknolojia nafuu
na zinazofaa ili kuongeza uwezo wa
wanawake wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani wa soko la ndani na nje.

Post a Comment