KESI YA MWANAMKE WA UGANDA ALIYEMEZA NA KUZIINGIZA ZANZIBAR KETE 38 ZA COCAINE YAENDELEA KUSIKILIZWA


 

NA MARYAM NASSOR.           

KESI ya mwanamke Raia wa Uganda aliyeingiza  madawa ya kulevya Zanzibar kete 38 zenye uzito wa gramu 454.208 inaendelea kusikilizwa katika Mahkama Kuu Tunguu Zanzibar.             

 Akitoa ushahidi wake shahidi namba mbili ambae ni sajenti wa polisi

kutoka Uwanja wa ndege wa Kimataifa Abeid Amani  Karume Zanzibar mbele ya Jaji wa Mahkama hiyo Mohamed Ali Mohamed na mwendesha mashtaka kutoka ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka Zanzibar Ali Amour na mawakili wawili wa Mshitakiwa ambao ni Ali Rashid na Elia Lesha Mgoya.   

Shahidi huyo, mwenye namba WP.5696 D/SGT Mtumwa  alieleza mahakamani  hapo kuwa  siku ya tarehe 22 Oktoba mwaka 2023 majira ya saa 8:10  huko uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume , uliopo kisauni Unguja alimkamatwa mtuhumiwa Jackie Ninsima  kwa shaka ya kuwa ameingiza  Dawa za Kulevya Zanzibar, na kupelekewa yeye kwavile ni Mwanamke mwenzake kwa ajili ya kumfanyia upekuzi mwilini mwake wakati anaendelea na upekuzi kwa Mwanamke huyo kilidondoka  kifurushi Cha chupi nyeupe ndani yake mukiwa na pipi 12 kati hizo pipi mbili zilikuwa kwenye kondomu.                                               

Sajenti Mtumwa, alidai kuwa baada ya hapo alimchukuwa mtuhumiwa huyo, na kumpeleka Hospitali ya Mnazi Mmoja Kwa ajili ya kufanyiwa kipimo cha CT SCAN na alionekana tumboni mwake Kuna vitu ambavyo si vya kawaida kuwemo ndani ya tumbo la Binaadamu , hivyo alilazwa hospitalini hapo akiwa chini ya Ulinzi wa SGT MTUMWA Kwa muda wa siku zote nne.  Ambapo Kwa siku ya kwanza alitoa Kwa njia ya haja kubwa pipi 17, na siku ya pili alitoa pipi nne na siku ya tatu pipi nne na siku ya mwisho alitoa pipi moja, Pipi zote hizo alizitoa kwa njia ya haja kubwa  na kufikia idadi ya pipi hizo kuwa 38.                                                                               

Awali mahkamani hapo alisikilizwa shahidi namba moja ambae ni Mohamed Hamduni Mohamed kutoka ofisi ya wakala wa maabara ya mkemia mkuu wa Serikali na kuthibitisha kuwa pipi hizo ni madawa ya kulevya aina ya cocaine yenya uzito wa gramu 454.208.                                                                             

Ilidaiwa mahkamani hapo kuwa Raia huyo wa Uganda mwenye Hati ya kusafiria (passport) yenye namba B00065972 alisafiri kwa ndege ya Ethiopian airlines kutoka Uganda  hadi Zanzibar kupitia Ethiopia.                                                                              

Mwanamke huyo,anashtakiwa Kwa Kosa la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Cocaine kete 38 zenye

uzito wa 454.208 kutoka Entebbe Uganda kuja Zanzibar, na kufanya hivyo ni kosa chini ya kifungu Cha 21 (1) (a) Cha Sheria ya mamlaka ya kuthibiti na kupambana na dawa za kulevya Zanzibar Sheria namba 8 ya mwaka 2021.  Sheria ya Zanzibar.                                                                                   

 Kesi hiyo imehairishwa hadi August 14 mwezi huu Kwa ajili ya kusikilizwa Kwa shahidi

namba tatu.

No comments

Powered by Blogger.