MTUHUMIWA WA KESI YA KUMUUWA MKEWE KWA KUKUSUDIA AENDELEA KUSOTA RUMANDE

 NA MARYAM NASSOR ,

MTUHUMIWA   wa kesi ya mauwaji, Khalfan Ali Abdallah( 26) amepandishwa katika kizimba cha Mahkama Kuu Tunguu  Zanzibar ,kwa tuhuma za kuua kwa makusudi chanzo kikitajwa ni wivu wa mapenzi.

Mara baada ya kufikishwa mahakamani hapo akitokea rumande na kusomewa shitaka lake hilo na mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar, Ali Amour Makame mshitakiwa huyo alikana shitaka hilo.

 Awali, Mwendesha Mashtaka huyo alimueleza Jaji wa mahakama kuu Zanzibar kuwa, kesi hiyo ni mpya na ipo kwa ajili ya Mshitakiwa kusomewa shitaka lake hilo.

Mara baada ya kusomewa kosa lake, Mshitakiwa Khalfan Ali Abdallah alikana kufanya kosa hilo la kumuua mkewe kwa makusudi.

“Muheshimiwa jaji, upelelezi wa kesi hii tayari umekamilika, Mshitakiwa leo hii hana wakili na hajaieleza Mahakama yako kuwa atakuwa na wakili au la, na kwa mujibu wa Sheria ya mwenendo wa Makosa ya Jinai ambayo ni sheria namba 7 ya mwaka 2018, katika kifungu cha 198 na 199 , kosa analoshitakiwa nalo ni kubwa na sheria hiyo inalazimisha mshitakiwa awe na wakili atakaemuwakilisha, hivyo tunaomba kesi hii ihairishwe na kuipanga tarehe nyengine ili kumpa muda  mtuhumiwa kutafuta  au kutafutiwa wakili kwa ajili ya kumsimamia kesi yake” alidai Mwendesha Mashtaka huyo.

Baada ya maelezo hayo, Jaji wa mahakama kuu Zanzibar  Ali Mohamed  alimuuliza mtuhumiwa huyo kuwa yuko tayari kwa ajili ya kuhairishiwa kesi yake hiyo na kujibu ndio.

 Kesi hiyo yenye namba 16/2024,kwa mara ya kwanza ilisomwa mahakamani hapo  juni 3   mwaka huu na kuhairishwa mpaka tarehe 27 mwezi huu, kwa ajili ya kuteuliwa washauri wa mahkama na kutolewa maelezo ya mashahidi mahakamani hapo.

Awali ilidaiwa mahakamani hapo  na Mwendesha Mashtaka, kuwa mstakiwa huyo  anadaiwa kumuua kwa makusudi  mkewe wa ndoa kwa sababu ya wivu  wa mapenzi.

Mshitakiwa huyo, alitenda kosa hilo, huko Bwejuu mkoa wa kusini Unguja majira ya saa 10:00  usiku.

Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, kutenda  hivyo ni kosa kinyume na kifungu  cha 179 na 180 chini ya  Sheria namba 6 cha mwaka 2018  sheria za Zanzibar.

Jaji, alisema kuwa mtuhumiwa huyo kutokana na shitaka lake hilo linalomkabili la kuua kwa makusudi  akithibitika na kosa hilo adhabu yake ni kunyongwa hadi kufa .

Kesi  hiyo,imehairisha hadi juni 27 mwaka huu kwa hatua ya kuteuliwa wasaidizi wa mahakama na kutolewa maelezo ya awali.

                                    MWISHO

 

 

No comments

Powered by Blogger.