UDHALILISHAJI KWENYE MICHEZO , SUALA LILILO SAHAULIWA
NA MARYAM
NASSOR, ZANZIBAR
WAANDISHI
wa habari na wadau mbali mbali, wamekuwa wakielimisha jamii, kuhusiana na suala
la udhalilishaji na ukatili wa kijinsia unaofanyika sehemu mbali mbali, ingawa wamekuwa
wakiisahau sekta ya michezo.
Katika michezo, kumekuwa kukifanyika
udhalilishaji na ukatili wa kijinsia, lakini mara nyingi, umekuwa ukifumbiwa
macho kwani watu wengi wamekuwa wakiinasibisha michezo na uhuni.
Lakini sio
kweli michezo ni afya na ndiyo sekta ambayo inaongoza kwa kutoa ajira
duniani, ikiwa watashirikishwa
vijana ipasavyo.
Hivi
karibuni, shirikisho la kandanda la nchini uhispania lilimshtaki Luis Rubiales,
Mkurugenzi wa zamani wa shirikisho hilo,
kwa kosa la unyanyasaji wa kingono.
Ambapo
ilikuwa ni kumpiga busu hadharani,
mchezaji wa timu ya wanawake Jean
Hermoso, alipokuwa akisherehekea ushindi wa kombe la dunia.
Busu hilo, ambalo Hermoso na wachezaji wenzake
walisema halikutakiwa na lilidhalilisha lilitokea katika ushindi waliyoupata dhidi ya
England baada ya kuwachapa
1-0 katika mashindano ya kombe la
dunia.
Wakati wa hafla ya kukabidhiwa kombe la dunia, Rubeales
alimshika kichwa cha Hermoso, katikati
ya mikono yake na kumpiga busu kwenye midomo yake.
Jaji wa mahakama kuu nchini Hispania, alisema pia Rubeales, anakabiliwa na shitaka la kulazimisha kashfa hiyona ikithibitika kosa hilo, hukumu yake ni mwaka mmoja jela.
Hiyo, ilikuwa ni ulaya, lakini hata barani
Afrika, bara lililojaa kila aina ya vipaji na wachezaji tumuangalie Caster
Semanya.
Semanya
ni mshindi wa mbio za mita 800 kutoka taifa la Afrika ya kusini mwenye
miaka 28, anakabiliwa na shindikizo la kimataifa la Olympik (IAAF) juu ya mpango wa kuwekewa masharti
magumu ya viwango vya juu vya
testosterone.
Chini ya
sheria za IAAF, mwanariadha wa kike mwenye viwango vya asili vya juu vya homoni
za testosterone, anatakiwa kukimbia na wanaume au kushiriki mashindano ya watu
waliyobadilishwa mpaka apate tiba ya kupunguza viwango hivyo.
Awali
Semanya, aliagizwa na wakuu wa riadhaa, afanyiwe vipimo vya jinsia ,lakini
hakuna matokeo yaliyotangazwa rasmi kwa
umma hadi sasa.
Zanzibar
kama ilivyokuwa sehemu nyingine duniani,
kumekuwa kukitokea vitendo vya
udhalilishaji kwenye michezo.
Ali Bakar
Ali ( si jina lake halisi) akizungumza na mwandishi wa makala haya alisema alishawahi kufanyiwa
kitendo cha udhalilishaji na kocha wake.
Alisema kuwa,
makocha ndio uti wa mgongo wa klabu, ingawa baadhi yao, hawana maadili mazuri
na kuharibu watoto.
“ Wakati
nacheza katika timu za chini ya umri wa miaka
15 kocha wangu, alinifanyia kitendo cha udhalilishaji,”alisema huku machozi
yakimtoka.
Aidha
alisema kuwa, lakini ni vigumu kuutambua udhalilishaji katika michezo kwani
hata wachezaji kwa wachezaji, hawalizungumzii suala hilo.
“Sisi wachezaji kwa wachezaji, hatuna ujasiri wa kulizungumzia suala hilo, kama tunafanyiwa udhalishaji na makocha au watu wengi kila mmoja anaweka siri kutokana na woga na kutojiamini kwake,’’anafafanua.
Aidha
alisema kuwa, wakati mwingine kocha, anawataka wachezaji kimapenzi, ndio
awapange kwenye kikosi na ukikataa unaweza usipate nafasi ya kucheza daima.
Haji Hamdu
Nahoda kocha wa timu ya Warrious ya wanawake alisema, wachezaji
wanakabiliwa na vitendo vingi vya
udhalilishaji na ukatili katika klabu zao.
Alisema
kuwa, lakini wachezaji wengi hawana elimu ya udhalilishaji, licha ya kuwa kesi za kwenye michezo haziingiliwi na
Serikali kwa baadhi yao.
Mrajisi wa
vyama vya michezo Zanzibar Abubakar Mohamed Lunda, alisema kuwa, wao ndio wenye
jukumu la kusimamia sheria na kanuni za
michezo kwa hapa Zanzibar.
Alisema kuwa, shirikisho la mpira wa
miguu (ZFF) wao ndio wanaoandaa na
kutunga miongozo na kuwapelekea ofisi ya Mrajisi, kwa kuitekeleza.
Aidha
alisema kuwa, kesi yoyote inayotokea ndani ya michezo inahukumiwa
kulingana na sheria za shirikisho la
mpira wa miguu la Afrika (CAF) na lile na kimataifa la (FIFA).
Alisema
ibara ya 58, ya katiba ya fifa inasema kesi yoyote inayotokea katika michezo
basi haitakiwi kupelekwa katika mahakama za kawaida au kwa maana nyIngine
Serikali, haitakiwi kuingilia kati.
Afisa
programu kutoka chama cha wanasheria wanawake Zanzibar (ZAFELA) Ruffea Juma, kwenye mradi wa michezo kwa
maendeleo unaodhaminiwa na shirika la
Ujerumani (GIZ) alisema wao wataandaa miongozo kwa wachezaji, ambayo
itatumika kama ni hamasa kwa wachezaji kuingia michezoni.
Mwandishi wa
habari mwandamizi Hauwra Shamte, hivi karibuni alipokuwa akiwapa mafunzo wandishi wa habari za michezo,
aliwataka kuripoti habari za usawa wa
kijinsia, katika michezo.
Aidha
alisema kuwa, wavulana na wasichana wanashindwa kufikia ndoto zao za kimichezo,
kutokana na vikwazo mbali mbali, ikiwemo vitendo vya udhalilishaji na ukatili
wa kijinsia katika michezo.
MWISHO
Post a Comment