KUTOKUWEPO KWA MIFUMO YA KIELETRONIKI MAHAKAMANI KUNAVYO WAKOSESHA HAKI , WATHIRIKA WA KESI ZA UDHALILISHAJI.
NA MARYAM NASSOR PEMBA,
MATUKIO ya
Udhalilishaji wa Watoto kama Ubakaji na Ulawiti si jambo geni visiwani
Zanzibar.
Visiwani humu, haiwezi kupita siku bila ya kusikia kwenye vyombo
vya habari vikitangaza kuhusu kesi za ubakaji na ulawiti .
Ikiwa si kusini, basi itakuwa kaskazini zimeripotiwa kutokana na
kushamiri kwake, lakini vitendo hivyo utavisikia tu.
Kwa kweli, ni jambo la kuchukiza sana, kutokea katika visiwa vya
Zanzibar, hasa kutokana na wananchi wanaoishi humu asilimia 99 ni waislamu.
Uislamu ni dini ambayo, inakataza vitendo viovu kama ubakaji na
ulawiti ambavyo hata ibilisi mwenyewe hawezi kuvifanya.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mwendesha Mashtaka Kutoka Afisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka Pemba, Ali Amour Makame alimweleza mwandishi wa makala
hii kuwa mwaka 2021 jumla ya kesi 64 za Udhalilishaji
ziliripotiwa Afisini kwao.
Kwa mwaka 2022, jumla ya kesi 48 za Udhalilishaji
ziliripotiwa, na kesi 26 ndizo zilizopatiwa hukumu na kesi 22 zilifutwa
Mahakamani kutokana na kukosekana kwa ushahidi.
Wakati kwa mwaka 2023 mpaka novemba, kuna kesi 48
ambazo zimeripotiwa na kesi 14 ndizo zilizopata hukumu.
Hadi novemba 2023, jumla ya kesi 7 ziliondolewa Mahakamani
kutokana na sababu ya kukosekana kwa ushahidi .
Na kesi sita, ziko tayari zinasubiri hukumu kutolewa na Hakimu wa
Mahakama hiyo Maalumu ya makosa ya Udhalilishaji.
Mwendesha Mashtaka huyo, alifafanua zaidi kwa kueleza kuwa kesi
nyingi hufutwa au kuondolewa Mahakamani kutokana na kukosa ushahidi.
Nilipomuliza wanalichukuliaje suala la kutokuwepo, Mazingira
rafiki Mahakamani kwa kesi za watoto alinijibu bila kusita.
Alisema, Mahakamani zogo ni kubwa, uhuru wa kuzungumza kwa
wathirika watoto bila ya kuwepo mtuhumiwa haupo.
Hivyo, “watoto wengi hushindwa kutowa ushahidi wao mbele ya Hakimu
kutokana na woga wa kumuangalia mtuhumiwa.”
Aliendelea kusema, yeye binafsi ana kesi ambayo hawezi kuisahau
hadi leo, ilitokea mwaka 2021 ya mtoto wa miaka mitano ambaye
alishindwa kutoa ushahidi Mahakamani.
Alisema, “kesi hiyo ilitokea Gombani Wilaya ya Chake
Chake Mkoa wa Kusini Pemba, mtoto alishindwa kutoa ushahidi wake kutokana na
hofu ya kumuona mtuhumiwa na kukumbuka vitisho vyake alivyompa.”
Hivyo aliongeza kwa kusema kuwa, Mahakama ilishindwa kupata
ushahidi kutokana na Mazingira yalivyokuwa si rafiki kwa kesi za watoto
hasa kesi za Udhalilishaji.
Aliongeza mwendesha mashtaka huyo, “kwa mantiki hiyo, ikitokea
mtoto ni mdogo na Mahakama hatumii video Conference, basi tunashindwa kupata
ushahidi.”
Alieleza changamoto hiyo hupelekea mzazi kukata tamaa kwa kuona
mwanawe anavyoteseka wakati wa kutoa
ushahidi kwa kukumbushiwa vidonda visivyo poa na kuamua kuiachia
kesi.
Nae, Mkurugenzi wa Jumuiya ya Tumaini Jipya (TUJIPE), Tatu
Abdallah Mselem alisema kesi nyingi za Udhalilishaji wa Watoto zinakosa
ushahidi Mahakamani kutokana na hofu kwa watoto.
Alisema, watoto bado hawajakomaa kiakili na
anapotendewa Udhalilishaji anapata athari kisaikolojia.
“Ukimwambia mtoto atowe ushahidi na yule mtu aliyemtendea anamuona
mbele yake, akikumbuka vitendo viovu anajawa na hofu na kushindwa kujielezea,”
alieleza mkurugenzi huyo.
Aidha aliongeza katika harakati zao za kutoa elimu ya kesi za
Udhalilishaji walikutana na mtu ambe mwanawe alifanjiyiwa Udhalilishaji ambapo
alilalamika kesi yake kufutwa Mahakamni kwa sababu ya kutoandikwa kwa miaka ya
muathirika wa Ubakaji ambae ni mwanawe.
Alimwambia mwandishi wa makala haya, “laiti Mahakama ingekuwa
inatumia video conference basi kesi nyingi zingepata hukumu kama inavyostahili
na mama yule angepata haki yake.”
Nae, Mrajisi wa Mahakama kuu Pemba, Faraji Shomari Juma, alikiri
kuwepo kwa changamoto ya uendeshaji wa kesi za watoto kwa Mkoa wa kusini
kutokana na tatizo la ushahidi kwenye kesi hizo.
Alisema, Mahakama hiyo kwasasa, haitumii mfumo wa kuendesha kesi
kwa kutumia teknolojia (video conference) kutokana na kuwa na
changamoto ya mfumo kutofanya kazi vizuri.
Aliongeza, “licha ya changamoto hiyo, tayari tumeshapata mfadhili
atakaye tusaidia kuweka sawa mfumo huo na kulitatua suala hilo karibuni.”
Tatu Abass Machano, ambae ni mshauri nasaha kituo cha Mkono kwa
Mkono Chake Chake, alisema anaamini ushahidi unakosekana kutokana na wathirika
kucheleweshwa kufika kituoni kwao kupata msaada wa kisaikolojia ili kumudu
kufuatilia kesi zao.
Alifahamisha kuwa, wathirika wengi wa kesi za ubakaji na ulawiti
ni watoto, hivyo wazazi huwachelewesha kuwapeleka jambo linalopelekea ushahidi
kuharibika.
“Kwa hatua za awali kama ushahidi haukuonekana na daktari, hata
ile michubuko haionekani vizuri kama mtoto kaingiliwa, hupelekea kukosekana kwa
ushahidi na kama hakuna ushahidi hakuwezi kuwa na kesi,” alieleza mtaalam huyo.
Katika hatua nyingine aliongeza kuwa changamoto hiyo inachochewa
zaidi na jamii kukosa uelewa wa kina kuhusu kesi za Udhalilishaji, kwani
waathirika wengi wanapelekwa vituoni tayari kasha poteza ushahidi muhimu
unaohitajika.
Nae, Mama wa mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji Asha Bakar Juma (si
jina lake halisi), alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kudai kuwa vitendo hivyo
vinaonekana kuongezeka kila siku kutokana na hukumu kuwa ndogo kwa watendaji.
Alimwambia mwaandishi wa makala hii kwamba kesi ya
mwanawe iliondolewa Mahakamani kutokana na kutoandikwa
umri katika jalada la kesi tu jambo ambalo lilizua mkanganyiko na kupelekea
mtoto wake kukosa haki yake.
Alisema, “Serikali ina nia thabiti katika kulitokomeza janga hili
la Udhalilishaji lakini Mahakama inarejesha nyuma.”
Aliitaka Serikali kuweka Mazingira mazuri katika Mahakama
Maalum za Udhalilishaji ili haki siyo tu itendeke bali ionekane
imetendeka kwa wote bila kujali hali ya mtu.
MWISHO.

Post a Comment