HAKIMU KASKAZINI UNGUJA, AZINDUA MUONGOZO WA JAJI MKUU ZNZ

 

 


NA MARYAM NASSOR,                          MAHKAMA  ya Mkoa wa kaskazini Unguja imezindua muongozo namba 1/2024 wa Mh.Jaji mkuu wa Zanzibar wa kuweka ukomo wa usikilizaji wa mashauri Mahkamani.

Akizungumza katika uzinduzi huo, huko Mahonda, hakimu  dhamana wa Mkoa wa kaskazini Unguja Lusiano Makoe Nyengo, alisema lengo la muongozo huo wa Jaji mkuu wa Zanzibar ni kuhakikisha  kuwa, mashauri  yote yanayofika Mahkamani yanamazilizika kwa wakati na haki inapatikana kwa wananchi.

Aidha, aliwasisitiza wananchi wa Mkoa wa Kaskazini kuiunga mkono  Mahkama kwa kuhakikisha wanakwenda Mahkamani kutoa ushahidi ili lengo la Mheshimiwa Jaji Mkuu la kuona kesi zinaendeshwa kwa haraka linafikiwa.

 

Akieleza, muongozo huo, lusiano alisema kwa Mahkama  za mikoa mashauri ya jinai  yasizidi  miezi 12  yawe yamemalizika, toka siku ya kwanza kufunguliwa.

Alisema kwa upande wa Mahkama za wilaya  mashauri ya madai na jinai yasizidi miezi sita, yawe yamemalizika toka siku ya kwanza kufunguliwa na mahkama za mwanzo  mashauri  yasizidi miezi mitatu, yawe  yamemalizika 

Kwa upande wake, kamanda wa Polisi mkoa wa Kaskazini Unguja Kamugisha, alisema jeshi la Polisi litashirikiana na Mahkama  kuona muongozo huo, unatekelezwa  kwa kuhakikisha wanaleta mashahidi Mahkamani na kukamilisha upelelezi,na kesi zimalizike kwa haraka.

Muendesha mashtaka dhamana wa Mkoa wa Kaskazini Unguja,Shumbana Mbwana , alisema  ili kufanikisha  muongozo huo,kunahitajika mashirikiano ya pamoja baina ya Mahkama, waendesha  mashtaka  na mawakili ili kumaliza kesi kwa haraka.

Uzinduzi wa muongozo huo, ulifanyika katika Mahkama ya mkoa Mahonda, ambao ulikwenda sambamba na kikao cha kusukuma mbele mashauri ya jinai.

                    MWISHO 

No comments

Powered by Blogger.