MGOMBEA URAIS ADC AHAIDI KUWATAFUTIA WAUME WANAWAKE WASIOOLEWA NDANI YA SIKU 100 AKIPEWA RIDHAA YA KUONGOZA ZANZIBAR.

 

Na Maryam Nassor

Mgombea Urais wa Serikali ya Zanzibar kupitia Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Hamad Rashid Mohamed, amesema endapo atachaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar  atahakikisha ndani ya siku 100 za mwanzo madarakani anawatafutia wanaume wanawake wote ambao hawajaolewa.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Kigunda, Jimbo la Nungwi, Wilaya ya Kaskazini A Unguja,  alisema hatua hiyo inalenga kupunguza vitendo vya udhalilishaji wa watoto vinavyosababishwa na ukosefu wa malezi bora katika jamii.

“Nikiwa Rais ndani ya siku 100 madarakani, wanawake wote ambao hawajaolewa nitawatafutia waume ili kupambana na vitendo vya udhalilishaji kwa watoto vinavyoendelea,” alisema Hamad.

Aidha, Hamad ameahidi kujenga barabara zote za ndani katika Jimbo la Nungwi endapo atapewa ridhaa ya kuongoza Zanzibar, akisisitiza kuwa wananchi wa eneo hilo watashuhudia mabadiliko ya kweli katika miundombinu.

“Tarehe 29 twendeni mkanichague mimi, Hamad Rashid Mohamed. Nawahakikishia nitawajengea barabara zote za ndani ambazo hazijajengwa,” aliongeza.

Aidha , aliahidi kujenga uwanja wa ndege wa Mkoa wa Kaskazini Unguja ulioko Nungwi, ili kurahisisha usafiri na kukuza shughuli za utalii katika eneo hilo.


 Alisema kuwa,  licha ya uwepo wa mahoteli mengi ya kitalii katika mkoa huo, vijana wa maeneo ya kaskazini hawapati ajira, jambo analoliona kama changamoto kubwa inayohitaji suluhisho la haraka.

“Tunajua changamoto zinazowakumba vijana wa Kaskazini A. Mmezungukwa na mahoteli, lakini hamna uhakika wa ajira  Ichagueni ADC ili iwahudumie,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wanawake wa Chama cha ADC, Nadhra Ali Haji, alilaani vikali tukio la kuchomwa moto kwa maskani ya chama hicho huko Kaskazini Pemba, akilitaja kuwa ni kitendo cha uvunjifu wa sheria.

“Hatutalifumbia macho jambo hilo, lakini tunawaachia Jeshi la Polisi wafanye kazi yao ya kuwatafuta wahalifu na kuwapeleka mbele ya sheria,” alisema Nadhra.

Naye Mgombea wa Ubunge wa Jimbo la Kigunda, aliwaomba wananchi kumpa kura ili aweze kununua gari la usafiri wa wanafunzi wa skuli katika eneo hilo, kutokana na changamoto ya usafiri inayowakabili watoto wa vijijini.

“Watoto wetu wanatembea umbali mrefu kufuata elimu, na wanapofika skuli vipindi tayari vimeshaanza. Nikichaguliwa, nitanunua gari maalum kwa ajili yao,” alisema.

Mbali na hilo, aliahidi pia kujenga uwanja wa mpira kwa vijana wa jimbo hilo, akisema kwa sasa wanatumia   kiwanja ambacho kipo katika mazingira hatarishi kwa shughuli za michezo.

Mwisho

No comments

Powered by Blogger.