Migogoro ya ndoa yazidi kuwaathiri watoto Zanzibar
NA NUSRA SHAABAN
ZANZIBAR inakabiliwa na ongezeko la talaka katika
familia nyingi, hali inayowaathiri moja kwa moja watoto waliozaliwa ndani ya
ndoa hizo.
Hayo yameibuliwa Katika mjadala wa wazi uliowakutanisha
wanawake, wanaharakati, walimu na wataalamu wa sheria kuhusu ndoa na familia
huko katika ukumbi wa Maji House Mjini Zanzibar.
Mwanasheria kutoka
Jumuiya ya Wanasheri Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Mwanaisha Mustafa
Makame, alisema wanaume kutowajibika ni
miongoni mwa sababu kubwa inayopelekea ongezeko la talaka visiwani humo.
Aliongeza kusema kuwa ripoti ya utekelezaji kutoka
ZAFELA inaonesha kuwa Jumla ya malalamiko 1,934 yakiwemo malalamiko ya
talaka,huduma,mirathi ,mgawanyo wa mali,idhini,cheti cha talaka,makaaazi ya
watoto,kubaka na kulawitiwa yaliripotiwa kwa mwaka jana.
Alisema kati ya malalamiko hayo, malalamiko ya ya talaka kwa mwaka 2024, yalikuwa ni 834, ambayo yalipelekwa
katika ngazi tofauti na mengine kupatiwa usuluhishaji.
Aliongeza kusema kuanzia mwaka wa 2025, malalamiko ya talaka yalipokelewa 344, ambapo mwezi wa Januari malalamiko ya talaka ni 72, mwezi Februari malalamiko ya talaka ni 78, mwezi Machi malalamiko ya talaka ni 68, mwezi wa April malalamiko ya talaka ni 50 na mwezi Mei ni 76.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa ZAFELA, Jamila Mahmoud Juma alisema elimu ndio mpango mzima, ipo haja watoto wakaandaliwa tangu wadogo kujitambua kimaadili na hata kufundishwa na mapema wakiwa skulini jinsi ya kuishi maisha ya utuuzima.
“Watoto wanawasikiliza sana walimu wao, ni wakati
sasa kwa kupitia mitaala iliyopo skulini, watoto kufundishwa adabu za ndoa na
mapema”alisema Jamila.
Naye Ukhty Amina Salum Khalfan,ni Afisa kutoka Wizara ya elimu ambaye pia ni
mwanaharakati wa masuala ya wanawake katika Uislamu, alisema jamii imeshindwa kujitambua na kuelewa dhamira
ya ndoa, ambayo ni makubaliano ya hiari yanayohitaji uvumilivu, majukumu ya
pamoja, na mshikamano.
Pamoja na hayo, Ukhty Amina alionya kuwa harakati
za kuwawezesha wanawake, japo zina faida nyingi, zinaweza kutumiwa vibaya na
kuwa kichocheo cha kuvunjika kwa ndoa.
Alieleza kuwa wanawake wanapopewa mamlaka bila
malezi ya kimaadili na kiroho, wanaweza kutumia haki yao ya kudai talaka kwa
misingi isiyo ya lazima.
Naye Omar Sheha Khamis Kadhi wa Mkoa wa Kusini
Unguja alieleza kuwa moja ya sababu
zinazochochea talaka ni matumizi mabaya ya mitandao na ushawishi wa vipindi vya
televisheni.
Alieleza
kuwa watoto na vijana wanajifunza kuhusu maisha ya ndoa kutoka kwenye tamthilia
na filamu zisizo na maadili, wakidhani kuwa ndoa ni ugomvi, kutengana na
matusi.
Aliongeza kuwa wazazi nao wanatelekeza majukumu
yao kwa kutumia muda mwingi kwenye simu badala ya kujenga misingi ya familia.
“Jamii turudi katika sheria ya ndoa ya kiislamu
kwa kuijua na kuifanyia kazi kwani, sheria ya ndoa ya kiislamu tayari
imeshafafanua na kuweka wazi kila kitu, tatizo liliopo ni sisi wenyewe
tunakiuka misingi iliyowekwa.” Alisema Sheikh Omar
Alitoa wito kwa viongozi wa dini na jamii kurudi
katika misingi ya mafundisho ya ndoa na kusema kuwa kuna haja ya kuzijadili upya aya za ndoa,
kuzifafanua kwa muktadha wa kizazi cha sasa, na kuhakikisha kuwa waumini
wanaelewa wajibu wao ndani ya ndoa.


Post a Comment