JACKIE NINSIME AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MAISHA JELA


NA MARYAM NASSOR

 MAHAKAMA Kuu  Zanzibar, imemuhukumu mshitakiwa Jackie Ninsime  mwenye umri wa miaka (47)  raia  wa  Uganda  kutumikia kifungo cha maisha chuo cha mafunzo kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya.

Akisoma  hukumu  hiyo,Jaji Mohamed  Ali Mohamed  amesema    mshtakiwa huyo ametiwa  hatiani  baada ya mahkama kujiridhisha  na Ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka .

 Amesema kuwa,  upande wa mashtaka ulifanikiwa kuthibitisha kosa hilo bila ya chembe ya shaka, kwa kuleta jumla ya   mashahidi sita  kutoa ushahidi wao mbele ya Mahkama hiyo.

“ Mahkama hii imejiridhisha na Ushahidi uliyotolewa na upande wa mashtaka  na  imemtia hatiani  mshtakiwa  huyo,  kutumikia kifungo cha maisha  chuo cha mafunzo ili iwe fundisho  kwake  na wengine wenye tabia kama hiyo .” amesema jaji Mohamed.

    Awali  Mahakamani hapo, Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar ( DPP) Ali Amour ,alidai kuwa   mshitakiwa huyo alikamatwa  Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Abeid Amani  Karume akitokea Uganda  kuja Zanzibar kwa ndege ya  Ethiopian Airline.

Aidha alidai kuwa, mshtakiwa huyo  uwanjani hapo  alishikwa na pipi 12 za  madawa ya kulevya  aina ya Cocaine, na pipi nyengine  26 zikiwa kazimeza na kuzitowa kwa njia ya haja kubwa akiwa katika hospital  kuu ya Mnazi mmoja  Unguja.

Awali ilidaiwa mahkamani hapo,  mshtakiwa huyo alishtakiwa kwa makosa ya kusafirisha na kumiliki madawa ya kulevya  aina ya Cocaine kinyume na kifungu namba. 21 (1) (a)  (d)  cha sheria  namba. 8 ya mwaka 2021 cha  sheria za Zanzibar.

 Ambapo ,  mnamo tarehe 22/10/2023 majira ya saa  nane na dakika tano mchana huko katika uwanja wa ndege  wa kimataifa wa  Abeid Amani Karume alipatikana akisafirisha  madawa ya kulevya aina ya Cocaine pipi 38 zenye uzito wa gramu  454.0258 jambo ambalo ni kosa kisheria.

 Kesi  hiyo ,ni ya tatu kwa mwaka huu kupata hukumu kubwa kama hiyo ya kifungo cha maisha jela  kwa kesi za madawa za kulevya  ya kwanza ilikuwa ni  ya Nassor Suleiman  Khalfani na wenzake wawili na ya pili ya Ali  Mohamed Ali maarufu Ali Macho na  Fahad Ali Khamis ambao walikamatwa na madawa ya kulevya na kuhukumiwa kifungo  cha maisha jela  .

         

                                    MWISHO

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

No comments

Powered by Blogger.