VYAMA VYA SIASA VIMETAKIWA KUWA NA SERA YA JINSIA ILI KUHAKIKISHA USAWA WA KIJINSIA
NA MARYAM
NASSOR
VYAMA vya
Siasa nchini vimetakiwa kuanzisha sera na madawati ya Jinsia katika vyama vyao ili kuhakikisha usawa wa kijinsia.
Ameyasema
hayo, Afisa mradi wa kuwawezesha wanawake katika maswala ya uongozi na haki za
kidemokrasia kutoka Chama cha Wandishi
wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ) Sabrina Yussuf alipokuwa akizungumza na
wawakilishi wa vyama 19 vya siasa nchini huko katika Ofisi
kuu za chama hicho Tunguu.
Amesema, lengo la mafunzo hayo ni kukuza ushiriki wa
wanawake katika maswala ya jinsia, na kuona namna gani vyama vya siasa vinatekeleza mikakati hiyo ipasavyo ili kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi .
“Mafunzo haya
yatawasaidia viongozi wa vyama vya siasa kuwa makini katika kuzitekeleza
sheria za vyama vya siasa nchini kwa kuanzisha dawati la jinsia na kukuza usawa wa kijinsia katika vyama vyao ,”
amesema .
Aidha
amesema kuwa, wameandaa mafunzo ya
viongozi wa vyama vya siasa kutokana na mabadiliko ya sheria ya uchaguzi ya mwaka 2024
kifungu no.10 C ambayo kinalazimisha kila chama cha siasa kuwa na sera ya jinsia ndani ya chama.
Amesema
kufuatia hatua hiyo, wameona ipo haja ya kuwapa
mafunzo viongozi hao ,ili wajuwe
namna gani wataazisha madawati ya jinsia ili kuhamasisha ushiriki wa wanawake
kugombea nafasi za uongozi.
“Tathimini
inaonesha bado wanawake wako kidogo
katika nafasi mbali mbali za uongozi
nchini , kwani mpaka sasa ni asilimia 37 tu ndio ambao wako katika baraza la wawakilishi”
anasema Sabrina.
Nae, Mkufunzi katika mafunzo hayo,Dk Sikujua Omar Hamdani
amevitaka vyama vya Siasa kuwa na sera Madhubuti
za kijinsia na utekelezaji wake ili kushajihisha ushiriki
wa wanawake katika kugombea nafasi za uongozi.
Amesema
kuwa, lazima vyama vya siasa viwe na
mikakati mbali mbali ya kuimarisha usawa wa kijinsia na kudhibiti vitendo vya
udhalilishaji wanavyotendewa wagombea wanawake.
“ Lazima vyama vya siasa kujidhatiti na kuwa na mikakati maalumu ya kuhamasisha wanawake kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili 50/50 ifikiwe” amesema Dk Sikuju.
Nae, mshiriki Suleiman
Ali Seif kutoka Chama cha Act
Wazalendo amesema suala la jinsia katika
chama chao limezingatia, kwani katika
baraza lao la Mawaziri kivuli limewashirikisha jinsia zote.
Amesema
kuwa, Chama chao kimekuwa kikihamasisha umuhimu wa dawati la jinsia ili kuwapa fursa wanawake kugombea kwa wengi
katika nafasi za uongozi.
Nae,
Salma Omar Saidi Katibu Idara ya Uchaguzi kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) anasema katika chama chao, sera ya
jinsia wanaitekeleza kwani kila nafasi itakayo
tokea wanapendekeza jinsia mbili kugombea.
“Sote
mashahidi katika chama chetu kuanzia viongozi wa ngazi ya Taifa hadi shina ni wanawake na
wanahamasisha pia wanawake kugombea katika kila nafasi ya uongozi” anasema.
Mafunzo hayo
ya siku mbili yaliyoandalia na Chama Cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar
(TAMWA ZNZ) , kwa kushirikiana na Chama
cha Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Jumuiya ya Wanawake wenye Ulemavu
Zanzibar ( JUWAUZA) na PEGAO kwa upande
wa Pemba kimewashirikisha viongozi wa vyama 19
vya siasa nchini na wandishi wa Habari.
Mwisho
Post a Comment