WANANCHI SHEHIA YA MAHONDA WAMETAKIWA KUUTUMIA MFUMO WA SEMA NA RAIS MWINYI ILI KUTATULIWA KERO ZAO

 

  


NA MARYAM NASSOR

WANANCHI wa shehia ya Mahonda wametakiwa kutoa malalamiko yao katika mfumo wa sema na Rais Mwinyi ili kutatuliwa matatizo yao yanayowakabili  katika sehemu husika.

 Akitoa elimu juu ya mfumo huo, naibu mkurugenzi  idara ya mawasiliano anayeshuhulikia maswala ya umma kitengo cha sema na Rais Mwinyi, Haji Khamis Makame huko katika Shehia ya Mahonda wilaya ya kaskazini ‘B’ Unguja.


Amesema  mfumo wa sema na Rais Mwinyi  ni takwa la wananchi, ambalo walilitoa wakati Rais Mwinyi alipokuwa akiomba kura kwa wananchi mwaka 2020.

Alisema kuwa, ndipo baada ya kushinda urais, akaamua kuanzisha kitengo hicho kwani hapo awali wananchi wa Zanzibar walisema hawana sehemu maalum ya kupeleka malalamiko yao  yanayowakabili na kupatiwa ufumbuzi, kwani wakipeleka kwa viongozi wa chini yanadharauliwa na hayafanyiwi kazi.

 Aidha amesema kuwa,  mfumo huo, umeanzishwa kwa lengo  la kusikilizwa na kutatuliwa kero za wanachi hivyo, ni vyema wakautumia ili kupatiwa ufumbuzi wa matatizo yao  yanayowakabili.

 Naibu mkurugenzi huyo, aliwatoa hofu wananchi wa shehia hiyo kuwa, mfumo huo unausiri na uhakika wa kutatuliwa changamoto za wananchi kwani tokea uwazishwe wamepokea malalamiko 17,000 na kuyafanyia kazi,na kila siku wanapokea malalamiko 25 kutoka kwa wananchi.

 Nae, sheha wa shehia ya Mahonda, Ali Issa Kinole aliwaasa wananchi wa shehia hiyo, kuendelea kutuma malalamiko yao katika mfumo huo, ili utumike kama ilivyokusudiwa.

Nae Mwananchi  Haji Fadhil alisema kuwa, wanamalalamiko  mengi kwa wizara ya mambo ya ndani ya nchi , kwani wanapoenda  kupeleka kesi kituo cha polisi wanaambiwa watie gari mafuta au wakamkamate mwizi wenyewe wampeleke kituoni.

‘’ Tukienda kituo cha Polisi kushtaki mfano kesi ya mwizi au ubakaji, tunaambiwa tutie gari mafuta au tukamkamate muhalifu wenyewe tumpeleke kituoni, sasa hatujui kuwa huo ndio utaratibu au laa’’ alisema.

Nae mwananchi,  Mussa Haji alisema kuwa jee katika mfumo huo malalamiko ya wananchi  yanamfikia kweli Muheshimiwa Rais au laa.

 Akijibu hoja za wananchi wa shehia hiyo, naibu mkurugenzi huyo aliwatoa hofu, wananchi hao na kuwataka kuripoti malalamiko yao katika mfumo huo, kwani yanashuhulikiwa na wahusika na kupatiwa ufumbuzi.

                   MWISHO

No comments

Powered by Blogger.